Pages

Nataka Kuokoka Sasa Hivi!

Ndugu yangu, hakuna kilicho bora sana duniani na baada ya maisha haya zaidi ya roho yako? Je, unafahamu baada ya maisha ya hapa duniani kuna maisha mengine ambayo wewe una maamuzi ya asilimia mia kuchagua?
Fahamu kuwa kuna Mbingu na Jehanamu. Mshahara wa dhambi daima ni mauti, na mshahara wa mema ni uzima wa milele. Chagua uzima ukaishi milele kwakuwa maisha ya hapa duniani ni ya kitambo kifupi sana nayo yamejaa masumbuko na taabu nyingi sana kila inapoitwa leo.
Yesu anakupenda sana, inawezekana kuna mtu anakupenda sana ila Yesu anakupenda zaidi ya wote duniani hivyo nakushauri ukate shauri umfuate yeye maana atakupa kustarehe milele na kuurithi ufalme wa mbinguni pamoja naye.

Tuesday, June 11, 2013

Mbegu Inakufa Ili Izae


Matunda mengi sana yanayoliwa hata yale yasiyoliwa yana mbegu moja au Zaidi ndani yake, na mbegu hizo zinaendeleza kizazi cha hilo tunda au muendelezo wa kuwepo kwa tunda kwa kadri maisha yanavyoendelea.
Mafanikio ya mbegu yoyote ni kuchipua ardhini hata ikawa mmea au mti uliokomaa na kuzaa matunda mazuri yatakayoiva, lakini mbegu isipofanikiwa kuchipua mti imeshindwa katika yote hivyo pia ilikuwa haifai maana kusudi lake hasa halijatimia.
Katika safari yetu ya kuelekea mbinguni haiwezekani kutenda mema na kumpendeza Mungu, zaidi sana kuwa watakatifu kama Yeye alivyo mtakatifu kama hatutakufa kwanza halafu tukafufuka, yaani ule utu wetu wa kale ambao unaambatana na tabia zote za asili hautazikwa ili tufufuke tukiwa viumbe wapya.
Yohana 3:3 – 7
Siku zote za maisha yetu inatupasa kujichunguza sana ili tujue pia kukubari mapungufu ndani yetu, yamkini tabia za asili bado zinatutawala. Mbegu inapofukiwa ardhini huwa inakufa kwanza hata iweze kuchipua upya. Unapoitizama mbegu iliyokufa (sio kuoza), lile ganda lake linakuwa limechoka na kuchakaa hata kushindwa kuzuia kile cha ndani yake kuchukua nafasi kutoka nje.
Miili yetu inapoachwa ikachakaa na kuchoka kabisa (kutokuhisi chochote kile cha dunia hii katika mwili wa nyama) ndipo pale tunapompa nafasi Roho wa Mungu akatawale na kutuongoza katika mema yote.
2 Wakorintho 5:17
Ipo mimea ambayo inadumaa, ama imechipua vema ila haizai matunda siku zote kiasi kwamba hatuipendi kwakuwa haina faida yoyote kwetu zaidi ya kuwa mmea au mti tu lakini kusudi lake hasa halijatimia, ndio maana tunapojichunguza inawezekana kabisa tumechipua lakini hatukui, au tunakua lakini hatuzai matunda wala hakuna dalili ya kuzaa matunda kwa sababu utu wetu wa kale bado umo ndani yetu, ama yamkini bado tunaipenda dunia kwa kiasi Fulani, na hatujataka kuiacha miili yetu ya nyama kufa kabisa.
Yohana 15:1 – 8
Siku zote mbegu inayopandwa katika udongo mzuri huzaa sana, vivyo hivyo nasi inatupasa tujiweke kwenye mazingira mazuri ya kukua kiroho, kuondokana na vishawishi vya tamaa na tabia za dunia hii kuchukua nafasi tena katika maisha yetu hata tukarudi nyuma kabisa ama kuwa vuguvugu.
Tunapokuwa kwenye mazingira sahihi ya kiroho na kimwili hakika tunauona utukufu wa Mungu ukituzunguka muda wote na kutawala maisha yetu, maana Mungu huwa hatuachi bali dhambi zetu wenyewe zinatutenganisha na uwepo wa Mungu, kama ambavyo mbegu iko tayari kufa ili ichipue tena na kuzaa lakini kuiteketeza mbegu ni kuiweka katika mazingira yasiyofaa.
Isaya 59:2

No comments:

Post a Comment