Pages

Nataka Kuokoka Sasa Hivi!

Ndugu yangu, hakuna kilicho bora sana duniani na baada ya maisha haya zaidi ya roho yako? Je, unafahamu baada ya maisha ya hapa duniani kuna maisha mengine ambayo wewe una maamuzi ya asilimia mia kuchagua?
Fahamu kuwa kuna Mbingu na Jehanamu. Mshahara wa dhambi daima ni mauti, na mshahara wa mema ni uzima wa milele. Chagua uzima ukaishi milele kwakuwa maisha ya hapa duniani ni ya kitambo kifupi sana nayo yamejaa masumbuko na taabu nyingi sana kila inapoitwa leo.
Yesu anakupenda sana, inawezekana kuna mtu anakupenda sana ila Yesu anakupenda zaidi ya wote duniani hivyo nakushauri ukate shauri umfuate yeye maana atakupa kustarehe milele na kuurithi ufalme wa mbinguni pamoja naye.

Tuesday, August 28, 2012

Leteni Hoja Zenye Nguvu



Unapomwendea mwajiri wako katika hitaji lako, huwezi ukaenda tu nakumwambia hitaji lako bali inakupasa uende ukiwa umejipanaga vema kukabiliana na maswali atakayokuuliza. Vivyo hivyo, hata mzazi anapopelekewa hitaji na mwanaye, atahitaji kufahamu umuhimu pia ulazima wa yeye kutimiza lile hitaji.
Ndivyo ilivyo hata kwa Baba yetu wa Mbinguni, ambaye siku zote anahitaji twende kwake tukiwa na hoja zenye Nguvu, ili tupate kupewa hitaji letu.
Isaya 41:21

Katika maisha yetu ya wokovu, inawezekana kabisa hatuendi katika utimilifu unaotakiwa ndio maana hata tunapokuwa na mahitaji ya msingi ya kuyapeleka kwa Mungu hatuwezi kupokea maana hatuna hoja za msingi hasa za kuzifungamanisha.
Hakuna mzazi ambaye anajua kabisa mtoto wake bado hajakua vya kutosha akaanza kumkabidhi majukumu mazito au kumpa nyenzo zilizo nje ya uwezo wake.

Hezekia alipougua, hoja yake ya msingi mbele za Mungu ilikuwa kumkumbusha Mungu jinsi ambavyo alikwenda mbele zake kwa ukamilifu wote, hata Mungu akakumbuka na kumponya tena akamuongezea miaka kumi na tano ya kuishi.
Isaya 38:1 – 6

Wengi wetu inawezekana tumeshakutana na fulsa mbalimbali wakati tunakua, ambazo pia huwa tunaziendeleza kwa watoto wetu. Mzazi anapomwambia mwanaye akifaulu mtihani atamnunulia zawadi au kitu anachokipenda sana, na ikawa mtoto akajitahidi na kufaulu mtihani basi mzazi anakuwa kwenye msukumo mkubwa wa kutimiza ahadi yake. Zaidi sana kwa Mungu wetu, tunapoenenda katika ukamilifu wote Naye atatimiza ahadi zake kwetu.

Isaya 43:26
Unakuwa na ujasiri sana unapokwenda mahali kudai haki yako, hasa unajua kwamba hakika hiyo ni haki yako, zaidi sana Mungu wetu anatupenda na kutujali kuliko hata wazazi wetu wa hapa duniani.
Bwana Yesu anasema kwamba tukimkiri Yeye mbele za mataifa, hakika naye atatukiri mbele za Baba yake aliye mbinguni.
Mathayo 10:32 – 33

Kuna siri moja ya kumkiri Yesu mbele za watu siku zote. Mungu anatutizama katika uhalisia kwamba sisi tumebeba taswira yake, hivyo tunapomkiri mbele za watu kwa matendo na maneno yetu tunampa msukumo wa Yeye kufanya kitu katika maisha yetu siku zote.

Hatasiku moja huwezi kurudisha bidhaa feki kwenye kampuni halali, maana inapofika pale wao hawaitambui kwasababu haiku kwenye nakala zao. Hivyo haiwezekani ukawa unamkiri Yesu kwa mdomo tu bila matendo ukategemea ujenge hoja za hapa na pale katika hitaji lako naye akupatie sawasawa na kuhitaji kwako.
Mathayo 7:22 – 23

Wednesday, August 22, 2012

Uraia wa Mbinguni



Ukiwa ni mkazi wa mji ambao wanaishi watu toka sehemu za tofauti mwa taifa, ni rahisi sana kumgundua mgeni anayetoka mkoa mwingine hasa kwa lafudhi yake pia lugha, na zaidi sana mavazi.
Lakini picha nzuri unaipata ukitembelea au kama unaishi nchi ya ugenini, maana kwanza unajiona mgeni eneo lile lakini pia inakuwa rahisi sana kumgundua mgeni mwingine au mwenyeji pia kwani katika mataifa yote ya dunia tunatofautiana sana katika mavazi, lugha pia lafundi hata kama lugha ni ile ile lakini zaidi sana hata rangi.

Mathayo 3:1 – 2
Mtu ambaye hajatubu, hayuko katika utayari wa kuupokea ufalme wa Mungu, maana hajatengeneza mazingira halisi ya kuishi katika ufalme wa Mungu. Lakini pia hata ambaye ametubu inawezekana kabisa bado hajaupokea ufalme wa Mungu ila ndio anaelekea.

Unapoomba uraia wa nchi nyingine kuna vitu vingi sana wanavyokufanyia usaili kwavyo; kama nchi unayotoka, historia yako, elimu yako, kazi yako na kipato, ukubwa wa familia yako pamoja na dhumuni lako katika nchi hiyo. Na ni pale unapomudu vigezo vyote ndipo utakapoweza kupata uraia wa nchi ile.

Mathayo 4:17
Bwana wetu, Yesu Kristo aliuleta ufalme wa Mungu hapa duniani, ili tuupokee na kuishi tukiongozwa na Roho Mtakatifu. Yesu ndiye mwanadamu pekee aliyeishi bila kutenda dhambi ingawa alijaribiwa hata zaidi ya tunavyojaribiwa leo hii.

Unapoupokea ufalme wa Mungu, kwako kuiba sio chaguo, wala kusema uongo si hatua ya kuifikia, tamaa haiwi tena sehemu ya maisha yako, ulevi wala uasherati vinakuwa si tena mvuto kwako zaidi kila kinachoitwa dhambi unakichukia sana maana unafurahi na kufarijika daima unapoishi katika ufalme wa Mungu. Hakuna mtu anayechukia nyumbani kwao, walipo ndugu na jamaa zake.
Raia wa nchi masikini anapokwenda kwenye nchi tajiri akafanikiwa sana na kupata kibali cha kuishi huko atafanya kila awezalo kuzishika na kutozivunja sheria za hiyo nchi kwani amepata sehemu ya furaha, faraja na amani pia.
Mathayo 13:44

Inatupasa tuutafute ufalme wa Mungu leo, maana inawezekana tumeokoka lakini bado tunashindana sana na dhambi kila inapoitwa leo, hata inafika wakati tunakata tamaa. Tufahamu kwamba kuokoka ni hatua ya msingi sana tuliyoifikia ila ili kumpendeza Mungu inabidi tuwe watakatifu, na hatuwezi kuwa watakatifu bila kuupokea ufalme Wake.
1 Peter 1:15 – 16

Mathayo 6:33 – 34
Tabia moja ya ufalme ni kuwa na kiongozi (mfalme) ambaye anahakikisha kila mtu anapata anachohitaji maana yeye ndiye anayemiliki wote na vyote. Sisi tunahangaikia sana maisha maana bado tunaamini sisi ni mali yetu wenyewe. Kama ambavyo mimi na wewe tunahudumia familia zetu je, si zaidi sana Baba yetu wa mbinguni?