Pages

Nataka Kuokoka Sasa Hivi!

Ndugu yangu, hakuna kilicho bora sana duniani na baada ya maisha haya zaidi ya roho yako? Je, unafahamu baada ya maisha ya hapa duniani kuna maisha mengine ambayo wewe una maamuzi ya asilimia mia kuchagua?
Fahamu kuwa kuna Mbingu na Jehanamu. Mshahara wa dhambi daima ni mauti, na mshahara wa mema ni uzima wa milele. Chagua uzima ukaishi milele kwakuwa maisha ya hapa duniani ni ya kitambo kifupi sana nayo yamejaa masumbuko na taabu nyingi sana kila inapoitwa leo.
Yesu anakupenda sana, inawezekana kuna mtu anakupenda sana ila Yesu anakupenda zaidi ya wote duniani hivyo nakushauri ukate shauri umfuate yeye maana atakupa kustarehe milele na kuurithi ufalme wa mbinguni pamoja naye.

Wednesday, November 30, 2011

MWAMBA WENYE IMARA



Mwamba wenye imara
Kwako nitajificha.
Maji hayo na damu
Yaliyotoka humu,
Hunisafi na dhambi,
Hunifanya mshindi.

Kwa kazi zote pia
Sitimizi sheria.
Nijapofanya bidii,
Nikilia na kudhii,
Hayaishi makosa;
Ndiwe wa kuokoa.
 
Sina cha mkononi,
Naja msalabani;
Nili tupu, nivike;
Ni mnyonge, nishike;
Nili mchafu naja,
Nioshe nisijafa.
 
Nikungojapo chini,
Na kwenda kaburini;
Nipaapo mbinguni,
Na kukwona enzini;
Roho yangu na iwe
Rahani mwako wewe.

Sunday, September 18, 2011

Niite Nami Nitakuitikia

Neno la Mungu liko wazi sana, anasema niite nami nitakuitikia nakukuongesha mambo makubwa magumu usiyoyajua.
Katika maisha yetu ya kila siku tunapitia nyakati mbali mbali zinazotuweka katika kuwaza na kutafakari sana kwakuwa ni hali ambazo ziko nje sana ya uwezo wetu wa kuamua na kutenda, na kwa jinsi hii kuna ndugu zetu ambao wamefikia wasaa wa kutamka kuwa hakuna Mungu wakiamini kama yupo basi kwanini wateseke namna hiyo?
Nimejifunza kitu cha msingi sana kwamba Mungu anatupenda wote, na hataki yeyote aumie wala kupotea ila anataka sote tumuendee yeye tukitenda mapenzi yake daima, pia maandiko yanatuambia kuwa Mungu wetu humrudi yule ampendaye. Mungu anaweza kuruhusu magumu yatufike ili tuweze kujongea karibu naye zaidi kwakuwa hakuna gumu lolote linalomshinda yeye, maana vyote tunavyoviona vilifanyika kwa neno lake.
Si mara zote kwamba tunapofikwa na mabaya tumemkosema Mungu, hasha! bali inawezekana kabisa ni mpango wa Mungu pia kuikuza imani yetu ili kuona uthabiti uliomo ndani yetu maana Ayubu alikutwa na jaribu ambalo alishinda na Mungu akamuinua zaidi. Tunamkumbuka baba wa imani, Ibrahim ambaye aliambiwa na Mungu amtoe Isaka kuwa sadaka ya kuteketeza, na Mungu alitaka kupima kiwango cha imani ya Ibrahim. Maandiko yanasema pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu daima.
Imani huja kwa kusikia neno la Mungu hivyo ikakuwa na kutenda mambo makuu. Neno la Mungu ni chakula cha roho, usipisoma na kusikia neno la Mungu, wewe ni sawa na mtu mfu maana roho yako haina uhai bali imekufa, hivyo kwa namna hiyo unaenenda daima katika mwili wala si katika roho. Mungu ni roho, ndio maana Yesu akasema wakati unakuja na sasa upo ambao wamwabuduo halisi watamwabudu katika roho na kweli. Pia akasema tukiwa na imani kama chembe ya haradali, tunaweza kuuambia mlima ng'oka ukatupwe baharini nao ukatii.
Mungu ni mwema sana, anatupenda kuliko vyote maana yeye ni baba yetu hata kumtoa mwanaye wa pekee ili aje ajishushe kuliko malaika, afe kwa ajili yetu kupata ukombozi wa dhambi. Inabidi tuache sasa kuenenda kwa mazoea na kumfuata Yesu na kulitii neno lake siku zote ili Mungu akapate kwenda kuonekana katika maisha yetu na zaidi ya yote atupe kuurithi ufalme wa mbinguni.
Kumbuka dhahabu husafishwa kwenye moto hata ikatoka inang'aa sana, vivyo hivyo majaribu ni mtaji wa kukua kwa imani zetu. Mungu akubariki sana!

Friday, August 19, 2011

Mtizame Mungu katika Uhalisia Mkuu

Mungu wetu ni Yule Yule jana, leo na hata milele. Habadiliki kwakuwa Yeye ni Alfa na Omega, Mwanzo na Mwisho.
Tunapokutana na shida, mtizamo wetu huwa ni namna gani kwa namna ya kibinadamu kwa nguvu, mali au maarifa yetu tunaweza kutatua tatizo, ambapo tunasahau kwamba hatuwezi neno lolote pasipo Mungu kuwa pamoja nasi. Maarifa ya binadamu kwa Mungu ni sawa na upumbavu!
Haijalishi katika nyakati hizi maarifa yamekua kiasi gani, ila ukweli ni kwamba bila pumzi ya Mungu sisi sio kitu chochote, pia maandiko yanasema mwanadamu ni udongo na kwenye udogo atarudi. Tukirejea pia Neno la Mungu linapotuambia nyakati hizi maarifa yanapoongezeka upendo wa wengi utapoa, na watu tutakuwa wenye kujipenda zaidi wenyewe, fedha, mali na anasa kuliko kumpenda Mungu.
Mungu ana namna nyingi sana za kutuongoza ikiwa pamoja na kuturudi kutokana na njia zetu mbaya ingawa katika uhalisia tunaona kwamba mengi tunayokutana nayo ni sehemu ya maisha ya kila siku ambayo yanampata yeyote yule ila wakati sasa umefika tumtizame Mungu katika uhalisia wake mkuu.
Mungu ni Yule Yule aliyemuongoza Yusufu katika magumu yote hadi kufikia ngazi ya juu ya utawala wa Misri, ndiye Yule Yule aliyembariki Jacob, akawavusha wana wa Israel kwenye bahari ya Sham, akawapa maji kwenye mwamba, akawashushia mana toka Mbinguni, aliyekuwa pamoja na Daudi mtumishi wake hata Daudi akamshida Goliati, ndiye aliyempatia Ibrahim mwana katika uzee wake.
Pia Mungu ndiye aliyeshusha gharika nyakati za Nuhu, pia akaiteketeza miji ya Sodoma na Gomora kutokana na kumuasi na kupitiliza kwenye dhambi kiasi cha kutisha.
Aliyetenda mema kipindi kile ndiye anayetenda pia anaweza kutenda leo hii, lakini tunapomuasi hawezi kuwa pamoja nasi hivyo mabaya yatatufika kwa urahisi sana. Mema yote hutoka kwa Mungu daima, kwakuwa yeye hutuwazia mema kila inapoitwa leo. Mabaya daima yanatoka kwa mwovu Shetani na malaika zake kwakuwa hiyo ndiyo asili yao.
Haijalishi ndugu yangu unasumbuka na kuteseka na mangapi; ila nakuambia leo kwamba usikate tamaa kumtumaini Mungu, maana pasipo imani haiwezi kumpendeza yeye hivyo ukiweka imani yako iwe thabiti mbele zake, daima utakwenda kuona uwepo wake kwako na Neno lake litakuongoza na baraka zikufike na kupitiliza kila uingiapo na utokapo.
Namna pekee ya kuongea na Mungu wetu ni kwa kupitia maombi, maana Yesu aliwaambia wanafunzi wake wakeshe wakiomba wasije kuingia majaribuni hivyo hatuna budi kuomba muda wote ili tufahamu Mungu ana mpango gani mbele yetu vinginevyo tutaenenda kama vipofu ambao wanajiongoza wenyewe na kuishia kwenye shimo.
Yamkini unathamini sana nyumba yako, gari, familia au kazi pengine elimu uliyonayo ila cha kusikitisha sana ni kwamba hakuna hata mmoja atakaye ondoka na kitu hata kimoja alichonacho hapa duniani wala kaviwezi kutusaidia kufika Mbinguni ila kwa kupitia Mwana pekee wa Mungu ambaye ni Yesu aliyekufa msalabani kwa ajili ya dhambi zetu. Tuna mifano mingi ya watu matajiri na wenye elimu sana waliokufa, ila miili yao ilizikwa bila mali yoyote. Ni vema kujifunza sasa kwa mifano hai na tukumbushane daima. Solomon anasema mambo yote chini ya jua ni ubatili mtupu!
Kuna wakati utafika ambapo kile utakachokuwa nacho ni ile hazina tu uliyoiweka Mbinguni kwa Baba, sasa je, unatumia kiasi gani kwenye starehe na anasa za duniani ambazo zinapita tu? Kumbuka, pasipo imani hatuwezi kumpendeza Mungu maana mkulima anapopanda mbegu anaamini kwamba udogo utaishikilia, mvua itanyesha na mazao yatashamiri walakini asingeamini hivyo asingepanda mbegu na kupoteza muda wake. Hebu kumbuka Ibrahim alimtoa mtoto pekee ambaye Mungu alimbariki naye katika uzee wake, lakini alijua kwamba Mungu alinipa hivyo hata nikimtolea atanipa tena.
Mimi na wewe si mali yetu wenyewe ila ni mali ya Mungu aliye hai, kwahiyo hatuna mamlaka wala ruhusa ya kufanya mambo yetu wenyewe ila kwa amri yake Yeye aliye Mkuu kuliko wote, maana kwa pumzi yake tunaishi, kwa neema na baraka zake tunafanikiwa daima. Usiogope wala kuwa na mashaka, ila amini kuwa Mungu habadiliki hivyo kama alitenda enzi zile, hata leo atatenda hivyo cha msingi ni kukaa katika Neno lake na kukua katika imani.
Baraka za Ibrahim, Isaka na Yakobo ziambatane nawe hata zikupitilize pamoja na vizazi vyako!

Monday, August 15, 2011

Kwanini Ni Ngumu Kusamehe na Kusahau?

Katika maisha yetu ya kila siku, tunakosea au kukosewa na wenzetu mara nyingi sana, ila zaidi ya yote tunamkosea pia Mungu wetu wa Mbinguni. Ni rahisi sana kuomba msamaha hasa pale tunapokosea wengine, tukitaka tusamehewe kabisa ila kwanini huwa inakuwa ngumu sana kwetu kusamehe na kusahau? Kama umesamehe lakini ujasahau je, huo ni msamaha halisia?
Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasamehe saba mara sabini, kwahiyo haijalishi ndugu yako kakukosea mara ngapi katika jambo moja au mambo tofauti ila inabidi kusamehe mara zote bila kuhesabu gharama na hiki ndicho kitu cha msingi sana maana tusipoweza kusamehe wenzetu tunaowaona hata Baba Yetu wa Mbinguni hataweza kutusamehe sisi makosa yetu.
Mara nyingi tukikosewa, hasira na kinyongo vinajengeka ndani ya mioyo yetu, na hii ni hatari sana kwasababu hatumpi utukufu Mungu hivyo hata roho wake hawezi kukaa sehemu yenye hasira, kinyongo, chuki wala husuda, Mungu wetu atusaidie sana.
Neno la Mungu linasema hasira hukaa kifuani mwa mpumbavu, ila zaidi ya yote hatutakiwi kukaa na hasira mpaka jua linapozama, na siku zote tukumbuke kuwa leo ni siku njema ambayo Mungu ameiumba hivyo tufurahi na kushukuru katika hiyo maana mbali na magumu yote tunayoyapitia tufahamu kuna wengi ambao walitamani kuwepo lakini hatuko nao tena. Kila leo ni zawadi toka kwa Bwana wa Majeshi.
Neno la Mungu linasisitiza pia kwamba ikitokea ukakwazika na kupatwa na hasira, daima usitende dhambi kutokana na hasira yako maana madhara yake ni makubwa sana. Inawezekana umehuzunika kiasi cha kukosa imani tena, una hasira kiasi cha kuishiwa nguvu hata ya kuomba na kuutafuta Uso wa Mungu wetu, Basi ni vema ukamshirikisha ndugu yako wa karibu sana kwa kadri Roho wa Mungu atakavyokuongoza ili akubebee mzigo wako katika maombi.
Bwana Yesu aliwaasa wanafunzi wake wakeshe wakiomba ili wasiingie majaribuni kwakuwa roho ila radhi ila mwili ni dhaifu. Maombi ndiyo silaha katika yote magumutunayokutana nayo siku zote za maisha yetu, na kwa Mungu hakuna gumu lolote asiloliweza.
Umuhimu wa kusamehe upo muda wote, ila si kusamehe tu bali kusamehe na kusahau maana Neno la Mungu linasema tazama ya kale yote wamepita na sasa yamekuwa mapya. Kwa hali ya kibinadamu ni ngumu sana hasa inapokuwa mtu anarudia kosa lile lile zaidi ya mara moja, na kwa jinsi hiyo tunakumbuka ni mara ngapi ambapo kosa hilo limekuwa likijirudia siku zote inatupa kuwa na wakati mgumu sana pia machungu moyoni, lakini Bwana Yesu amesema nira yake ni laini na mzigo wake ni mwepesi hivyo tukimbilie kwake tupate pumziko.
Tatizo la kutosamehe toka moyoni ni la kila mtu katika ulimwengu wa sasa, lakini Neno la Mungu linatuasa kutafuta kwa bidii kuwa na amani na watu wote pamoja na huo utakatifu kwakuwa hakuna atakaye muona Mungu asipokuwa nao. Katika nyakati hizi, hatutakiwi kuweka hasira wala kinyongo kwakuwa hatujui lini Yesu atarudi kulinyakua kanisa au ni wakati gani kifo kitatukuta maana hakuna dhambi ndogo wala kubwa ila yoyote ile inatosha sana kukupeleka kwenye ziwa liwakalo moto milele na milele.
Kila tunapoomba Mungu anasikia, naye Baba yetu yuko tayari kutupa msaada muda na wakati wote kama tukikiri kutokuweza na kwenda mbele zake kwa toba ya kweli. Inatupasa kuwapenda adui zetu, kuwaheshimu na kujishusha kwako, yamkini tunatizama kibanzi ndani ya jicho la jirani badala ya kuitizama na kuitoa boriti kwenye jicho letu kwanza.
Mungu atusaidie siku zote tuishi maisha yanayompendeza yeye pamoja na wanadamu wote ili baraka zake zisitupungukie ila zitufikie hata zitupitilize, kwakuwa hatutachoka kutenda mema siku zote za maisha yetu.
Upendo na Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe pamoja nasi siku zote za maisha yetu na Mungu atubariki sana.




Monday, August 1, 2011

Usigeuke Nyuma na Kumuacha Yesu






Mke wa Lutu aligeuka hakuweza kuvumilia wala kuamini kwamba yale yote waliyoyaacha Sodoma yalikuwa yakiteketea, pia inawezekana kabisa alikwenda mwendo mrefu akijishauri kugeuka atazame au lah, lakini mwishoni akakata shauri na kuamua kugeuka nyuma.
Ama kwa hakika neno la Mungu ni kweli tena lazima litimie, na kwakuwa alikiuka agizo walilopewa na malaika, mara tu baada ya kugeuka nyuma alibadirika na kuwa nguzo ya chumvi, na hapo ndipo mwisho wake ulipokuwa.
Shetani daima ni mshawishi ambaye hawezi kukushawishi mema hata siku moja, kwakuwa yeye huja kuua na kuharibu ila Yesu alikuja ili tuwe na uzima tena tuwe nao tele. Mke wa Lutu alitamani tena yale ya Sodoma, yawezekana alikumbuka jamaa zake, au mali zao zote walizokuwanazo, lakini sawa sawa na neno la Mungu kwamba rafiki wa dunia hawezi kumpendeza yeye hata siku moja.
Bwana Yesu anatuasa kuachana na vyote kisha tujitwike msalaba wetu na kumfuata maana vyote vya duniani vinapita tu kwakuwa tulizaliwa uchi tukiwa hatuna chochote pia tutaondoka tukiwa hatuna chochote. Huu ni uhalisia ambao shetani ametuficha wengi sana tunaohangaika na dunia hii na kumsahau Mungu wetu anayetuambia tuutafute ufalme wake kwanza na haki yake kisha yote tutazidishiwa maana fedha na dhahabu vote ni mali yake Bwana wa Majeshi.