Pages

Nataka Kuokoka Sasa Hivi!

Ndugu yangu, hakuna kilicho bora sana duniani na baada ya maisha haya zaidi ya roho yako? Je, unafahamu baada ya maisha ya hapa duniani kuna maisha mengine ambayo wewe una maamuzi ya asilimia mia kuchagua?
Fahamu kuwa kuna Mbingu na Jehanamu. Mshahara wa dhambi daima ni mauti, na mshahara wa mema ni uzima wa milele. Chagua uzima ukaishi milele kwakuwa maisha ya hapa duniani ni ya kitambo kifupi sana nayo yamejaa masumbuko na taabu nyingi sana kila inapoitwa leo.
Yesu anakupenda sana, inawezekana kuna mtu anakupenda sana ila Yesu anakupenda zaidi ya wote duniani hivyo nakushauri ukate shauri umfuate yeye maana atakupa kustarehe milele na kuurithi ufalme wa mbinguni pamoja naye.

Monday, June 24, 2013

Hesabu Baraka


Maisha yetu kwa sehemu kubwa sana yamejawa na mtazamo wa kutizama ni kipi ambacho hatuna, ama ni wapi ambapo tunahangaika daima. Hakika duniani tunayo dhiki, lakini katika uhalisia tumebarikiwa sana kuliko dhiki tulizonazo, zaidi sana dhiki yetu ni ya kitambo kifupi tu.
Tunapohesabu baraka, tunaruhusu ukuu na uweza wa Mungu uonekane katika maisha yetu siku zote, zaidi tunaweza kuona na kujua kuwa Mungu yuko kazini akijishughulisha kwa ajili ya mambo yetu kuliko ambavyo tunaweza kutafakari na kuona.
Zaburi 100:4
Ukimtizama mtoto mdogo, anajua kuwa kila kitu kipo, tena anajua kuwa baba ana pesa ya kutosha kumnunulia kila anachohitaji, ndio maana siku zote watoto wana furaha na amani. Lakini pia watoto hawajui kupima uzito wa mahitaji muhimu, hivyo hatutakiwi kuwa kama watoto katika hili bali tutafakari siku zote mema ambayo Mungu ametufanyia na kushukuru tukimsifu daima.
Kubarikiwa si kuwa na majumba ya kifahari, wala magari na pesa nyingi bali kuwa mzima mwenye afya tele pamoja na amani ipitilizayo amani zote tukipata kibali kila tuendapo. Kubarikiwa pia ni kumjua sana Mungu tukizishika amri zake.
Ayubu 22:21
Mtu anapobarikiwa na Mungu, anatosheka anakuwa hana uhitaji tena, ndio maana Bwana Yesu alimwambia yule mwanamke Msamaria kuwa akinywa maji atakayompa Yeye hakika hataona kiu tena. Kitu chochote kile kilichobarikiwa na Mungu kinatosha kabisa wala hakihitaji nyongeza. Lakini tunapokuwa na mali ama utajiri ila tunahitaji kupata zaidi inabidi tujikague na kumuuliza Mungu kuwa ni baraka toka kwake au lah, kwa maana wengi wameacha kumuabudu Mungu wakaabudu mali na utajiri.
Yakobo 3:10
Mungu ametupa uwezo wa kujitamkia na kuwatamkia wengine laana au baraka, lakini mara nyingi tunatumia ndimi wetu kulaani badala ya kubariki. Mara nyingi tunajiambia kwamba hii kazi ikiisha sijui itakuwaje, ama siwezi kufanya biashara, au mke wangu ni mkorofi sana, ama watoto wangu ni wakaidi mno, au sidhani kama nitafanikiwa daima pamoja na mengine mengi. Haya pia huwa tunayazungumza kwa wengine hata tukawalaani.
Warumi 12:2
Kwa Mungu wetu hakuna laana, wala magomvi yoyote bali kuna amani, upendo, upole pamoja na baraka tele. Mataifa huenenda wakitizama nini au kipi wanakosa na wapi wamepungukiwa wakizidi kuona kwamba hakika maisha hayawatendei haki, bali sisi si wa dunia tena na haitupasi kuenenda kama wao.
Wafilipi 4:8
Inatupasa kutambua baraka zetu kama jinsi ambavyo zinatuzunguka, lakini pia inatubidi kukiri baraka hata kabla hatujaziona kwa macho ya nyama, cha msingi tumeshamuomba MUngu na kuamini hakika itakuwa sawa sawa na kuamini kwetu.

No comments:

Post a Comment